Saturday, June 1, 2013

WAUMINI WAUKIMBIA MSIKITI WA DODOMA BAADA YA KAULI YA MBUNGE KUDAI KUWA UNAFUNDISHA UGAIDI


Kauli iliyotolewa na mbunge wa kilindi Beatrice Shelukindo ya kuwa msikiti wa barabara ya saba uliopo katika manispaa ya Dodoma unafundisha mafunzo ya ugaidi na kareti kwa waumini wake imeuathiri msikiti huo.
Akizungumza na Jombo Shekhe Mohamed Awadhi wa msikiti huo alisema kauli yake hiyo Imewaathiri waumini wake kutokana kuukimbia na baadhi ya wanafunzi waliokuwa wakisoma masomo kuhamishwa na wazazi wao.
Awadhi alisema hivi sasa wapo katika wakati mgumu kutokana na waumini waliokuwa wakiswali ndani ya msikiti huo kuamua kuhama baada ya kutolewa kauli ambayo wanaamini ni ya uzushi na uchochezi kwa ajili ya kupotosha jamii na serikali.
Shekhe huyo alisema kuwa msikiti huo umejengwa kwa miaka mingi na karibu baadhi ya wanaoswali ni pamoja na viongozi wa kiserikali wakiwemo askari toka taasisi mbalimbali kama vile polisi,wanajeshi,usalama na takukuru.
“Sasa kama kweli sisi tungekuwa tunafundisha hayo mafunzo ya ugaidi na kareti,serikali pamoja na waumini kutoka vyombo vya dola kweli msikiti huo ungeachwa bila kuchukuliwa hatua zozote”aliuliza Shekhe Awadhi.
Naye mlezi wa wanafunzi wa msikiti huo wa barabara ya saba Husseni Hamedi Fundi,alikiri baadhi ya wazazi na walezi kuwahamisha watoto wao kutokana na kauli iliyotolewa na mbunge huyo wa jimbo la Kilindi.
Fundi alisema kuwa msikiti unapokea wanafunzi kutoka nje ya Mkoa wa Dodoma kama vile Kigoma,Singida,Mwanza,Pemba,Zanzibar,Tanga na Bukoba kwa ajili ya kujifunza  lugha ya kiarabu na elimu ya Quran.
“Lakini hivi sasa baadhi yao wamehamishwa na wazazi, walezi na hii yote ni kutokana na uzushi uliotolewa na Mbunge huyo wa Kilindi ambaye sisi kama waumini wa msikiti huo tunaona amepotosha jamii na serikali yetu,
''Kauli yake hiyo imetudhalilisha sana hivyo tunaamini Mwanamama huyo anatakiwa kusema ukweli ukizingatia kuwa sehemu anayoielezea ni Bunge ambalo linalotegemewa na Watanzania wote'', Alisema Fundi
Kauli hiyo iliyoleta utata ilitolewa na Mbunge wa  jimbo la Kilindi Beatrice Shelukindo mei 4, mwaka huu wakati akichangia bajeti ya Wizara ya mambo ya ndani alisema msikiti huo wa barabara ya saba unatoa mafunzo ya ugaidi na kareti.

  CREDIT: RICHARD MWAIKEND

No comments:

Post a Comment